IQNA

Maafisa wa polisi wa kike Trinidad na Tobago washinda haki ya kuvaa Hijabu

20:53 - November 11, 2018
Habari ID: 3471738
TEHRAN (IQNA) - Mahakama Kuu ya Trinidad na Tobago imetoa hukumu ya kuwaruhusu kuvaa Hijabu maafisa wa polisi wa kike ambao ni Waislamu.

Hukumu hiyo imetolewa na Jaji Margaret Mohammed kufuatia kesi ya kikatiba dhidi ya serikali iliyowasilishwa na Sharon Roop (kwenye picha) akitaka kuruhusiwa kuvaa hijabu wakati akiwa kazini kama afisa wa polisi.
Katika hukumu yake, Jaji Mohammed amesema hatua ya serikali kumzuia Roop kuvaa Hijabu akiwa kazini ni jambo ambalo limekiuka uhuru wake wa imani.
Aidha jaji huyo ameitaka serikali imlipe polisi huyo fidia ya hasara zote ambazo amepata wakati wa kusikilizwa kesi yake.
Hukumu hiyo inamaanisha kuwa serikali ya Trinidad na Tobago italazimika kufanya mabadiliko Sheria za Huduma ya Polisi ili kuwaruhusu wanawake Waislamu ambao ni maafisa wa polisi kujumuisha Hijabu kama sare rasmi.
Jamhuri ya Trinidad na Tobago ni nchi ya visiwani katika Karibi ya kusini, karibu na pwani ya Venezuela, kusini kwa kisiwa cha Grenada cha Antili Ndogo. Nchi jirani nyingine kuvukia bahari ni Barbados na Guyana. Waislamu ni asilimia 5 ya watu milioni 1.2 wa nchi hiyo.

3467180

captcha