Mnamo Novemba 23 mwaka huu, mji wa Osaka ulipata haki ya kuandaa maonyesho ya kimataifa ya World Expo 2025 ambayo yanatarajiwa kuwavutia wageni milioni 28 kutoka kote duniani.
Kwa msingi huo wakuu wa mji huo wameanzisha mikakati maalumu ya kuhakikisha kuwa Waislamu wanapata bidhaa na huduma kwa mujibu mafundisho ya Uislamu.
Ammar Jebawi, mwanzilishi wa Jumuiya ya Halal ya Nishi Nippon anasema kutafanyika mabadiliko makubwa mjini Osaka kabla ya maonyesho hayo na hivyo sekta ya Halal inajitahidi kuhakikisha wageni Waislamu wanapata huduma kwa mujibu wa mafundisho ya dini yao.
Mbali na Osaka, mji mkuu wa Japan, Tokyo, ambao utakuwa mwenyeji wa Michezo ya Olimpiki yam waka 2020, nao pia unatekeleza sera maalumu za kutoa huduma na chakula halali kwa wakaazi, watalii, wanamichezo na wafanyabiashara Waislamu. Idadi kubwa ya watalii Waislamu wanaotembelea Japan ni kutoka nchi kama vile Malaysia, Indonesia na nchi za Kiarabu.