Mahakama imesema imekubali ombi la gavana wa jimbo hilo la kupelekwa Sheikh Zakzaky na mkewe katika jela kuu ya jimbo hilo.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Nigeria, Mahakama Kuu ya jimbo la Kaduna imechukua uamuzi usiotarajiwa wa kukubali kupelekwa kwenye jela kuu ya jimbo hilo Sheikh Ibrahim Zakzaky na mkewe baada ya kuombwa kufanya hivyo na gavana wa Kaduna.
Hivi sasa Mkuu huyo wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria anashikiliwa sehemu isiyojulikana na kwa mujibu wa taarifa za uhakika, Sheikh Zakzaky anasumbuliwa na matatizo mengi ya kiafya.
Mahakama Kuu ya Kadunia hata haikugusia japo kwa mbali suala la hali ya kiafya ya sheikh huyo mwanaharakati.
Mwezi Agosti mwaka huu, Sheikh Ibrahim Zakzaky alipelekwa India kwa matibabu lakini maafisa usalama wa serikali ya Nigeria walimuwekea vizuizi vingi na walimtishia hata kumuua, hivyo alilazimika kurejea Nigeria bila ya kufanyiwa matibabu yoyote.
Vikosi vya usalama vya Nigeria vilimchukua Sheikh Zakzaky na mkewe mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa mji mkuu Abuja na kumpeleka kusikojulikana.
Sheikh Ibrahim Zakzaky, Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu Nigeria na mkewe walitiwa nguvuni tarehe 13 Desemba 2015 wakati askari wa jeshi la Nigeria walipovamia na kushambulia Hussainiyah iliyoko katika mji wa Zaria. Katika shambulio hilo, mamia ya Waislamu wa madhehebu ya Shia nchini Nigeria, wakiwemo wana watatu wa kiume wa Sheikh Zakzaky, waliuawa shahidi.