Serikali ya Nigeria imetangaza kuwa kwa akali wanachama 100 wa kundi la kigaidi la Boko Haram wameangamizwa katika operesheni dhidi ya ugaidi iliyotekelezwa na jeshi la nchi hiyo.
Kamandi ya kijeshi dhidi ya ugaidi nchini humo imesema kuwa, katika operesheni hiyo ambayo imetekelezwa katika jimbo la Borno, askari 28 wameuawa na wengine 61 kujeruhiwa. Baadhi ya duru zimedokeza kuwa kuwa wanajeshi 70 wa Nigeria wameuawa katika mapigano hayo.
Kwa mujibu wa kituo cha masuala ya haki za binaadamu cha Umoja wa Mataifa, kutokana na mashambulizi ya kigaidi ya genge la Boko Haram hadi sasa zaidi ya watu elfu 30 nchini Nigeria wameuawa na karibu milioni tatu wamekuwa wakimbizi.
Kundi la kigaidi la Boko Haram lilianzisha ugaidi wake huko eneo la kaskazini mashariki mwa Nigera mwaka 2009. Hata hivyo lilipanua shughuli zake taratibu hadi katika nchi jirani za Kiafrika zikiwemo Niger, Chad na Cameroon.